loader image

Tigo pesa TnC

Vigezo & Masharti ya Tigo Pesa 

Vigezo na Masharti haya yametolewa na MIC Tanzania Public Limited Company na yatatumika kwa wateja wote wa Huduma za Tigo Pesa. 

MAANA ZA MANENO

Mteja: Ina maana ya mtu au taasisi ambayo imejisajili kikamilifu na inaweza kutumia huduma yoyote ya Tigo Pesa kupitia mfumo wowote.  Neno “Mteja” linajumuisha wawalikilishi binafsi wa mteja husika, warithi wa cheo chake na wasaidizi pamoja na watu ambao ni watendaji wenye mamlaka kwa wateja kama vile wakala, wahudumu au wafanyakazi.

Akaunti: Ina maana ya kumbukumbu ya MIC ya taarifa binafsi, gharama zinazopaswa kulipwa na malipo yanayopokelewa kutoka kwa Mteja kupitia Kadi hai ya Simu.

Mwenye Akaunti: Ina maanisha Mteja.

Kadi hai ya Simu: Ina maanisha Kadi ya Simu ambayo huduma ya Tigo Pesa imewezeshwa na inafanyika kupitia Kadi hiyo ya Simu mara kwa mara kama ilivyoelezwa katika sheria za utumiaji.

Tarehe ya Kuanza Kutumia:   Ina maana ya tarehe ambayo Mteja alifanikiwa kujiunga na kuwa na uwezo wa kutumia Huduma ya Tigo Pesa.

Gharama: Ina maana ya gharama/ada za matumizi ya Huduma ya Tigo Pesa kama itakavyokuwa imeamuriwa na kutangazwa na MIC.

Mkataba: Ina maana ya vigezo na masharti haya na kadri yatakavyokuwa yanafanyiwa marekebisho mara kwa mara kwa maandishi na MIC.

Uunganishaji: Ina maana ya utaratibu ambao unamuwezesha Mteja kupata huduma ya Tigo Pesa kupitia mtandao wa MIC. Neno “Kuunganishwa”, “Kutokuunganishwa” na “Kuunganishwa tena” lina maana ya hadhi ya kuunganishwa kwa Mteja.  Kuunganishwa ina maana iko hai na inafanya miamala, Kutokuunganishwa ina maana haiko hai katika kipindi kinachohusika wakati Kuunganishwa tena ina maana kuwa imebadilisha hadhi kutoka kutokuunganishwa kwenda kuunganishwa.

MIC:  Ina maana ya MIC Tanzania Public Limited Company yenye ofisi yake iliyosajiliwa katika jengo la Derm Complex, Plot No. 11 Block 45A, Barabara ya Bagamoyo, Eneo la Kijitonyama, Dar- es- Salaam, Tanzania.

Tigo:  Alama ya kibiashara iliyosajiliwa ya MIC kwaajili ya kutolea huduma zake.  Maneno MIC na Tigo yanaweza kutumiwa kwa kubadilishana kuwakilisha kampuni.

Simu ya Mkononi: Ina maana ya kifaa kichonaweza kupiga na kupokea simu kupitia mawimbi ya redio wakati ukiwa unatembea katika eneo pana la kijiografia.

Mtandao: Ina maana ya vifaa vya MIC programu na mitambo ambayo inamuwezesha Mteja anayetumia simu ya mkononi inayokubaliana na GSM 900,1800 na 2100 au mfumo mwingine wowote unaotumiwa na MIC {isipokuwa SIM iliyofungwa na kampuni nyingine ya simu} kuweza kupata huduma.

Namba ya Siri:  Ina maania namba ya pekee ya utambulisho binafsi  inayotumiwa na Mteja kupata huduma ya Tigo Pesa.

Haki: Ina maana haki miliki ya nembo ya biashara na miliki zingine zinazohusika na haki za uvumbuzi zinazohusiana na yaliyomo au yaliyoko katika programu yoyote ambayo inahitajika na/au inatumiwa na MIC kuendesha Mtandao na kutoa huduma ya Tigo Pesa.

Huduma ya Tigo Pesa/Huduma ya Kifedha kwa Simu za Mkononi: Ina maana ya huduma inayotolewa na Tigo yautoaji na upokeaji fedha za kielektroniki na utumaji wa fedha za kielektroniki kati ya Wateja kwa misingi ya uhamishaji wa maelekezo ikiwemo taarifa za miamala yote, kuthibitisha na kuhakikisha miamala yote inajumuishwa na kusasisha taarifa za akaunti ya Mteja.   

AML/CFT:  Inarejelea katika Utakatishaji wa fedha na Kufadhili Ugaidi kama ambavyo imetafsiriwa na sheria za Tanzania.

Utakatishaji waFedha: Inajumuisha kuchukua fedha zitokanazo na uhalifu na kuficha vyanzo vyake visivyo halali ili kutumia fedha hizo kufanya shughuli halali au zisizo halali. 

Kufadhili Ugaidi: Inarejea katika utaratibu wa kutoa fedha au msaada wa kifedha kwa magaidi au makundi ya ugaidi kwa kutumia fedha kutoka katika vyanzo halali au visivyo halali. 

KADI ZA SIMU:  Ina maana ya Moduli ya Ubainishaji wa Mteja ambayo hutolewa na MIC kwa  Mteja kumsaidia Mteja kupata na kutumia mtandao na Huduma zinazohusika. 

“Wakala (mawakala) ina maana ya mtu au watu waliosajiliwa au waliopewa kibali na Tigo  kutoa huduma ya Tigo Pesa kama vile kutoa na kupokea fedha taslimu.

 

  1. KUANZA NA VIGEZO NA MASHARTI

Vigezo na masharti haya yatatumika kwa Mteja mara tu baada ya kujiandikisha katika huduma ya Tigo Pesa na yataendelea kutumika wakati wote ambapo mteja atakuwa anatumia Huduma ya Tigo Pesa mpaka pale ambapo akaunti ya Tigo Pesa itakapofungwa.  

 

  1. KUJIUNGA NA HUDUMA YA TIGO PESA 

Mteja atajiunga na huduma ya Tigo Pesa kwanza kwa kusajili kadi yake ya simu kwa kutumia utaratibu wa kampuni wa kusajili kadi za simu wakati atakapokuwa ameshakidhi masharti ya usajili wa kadi ya simu.  Fomu ya kusajili wa Mteja itatofautiana kutegemeana na hali ya kisheria ya Mteja (kama ni Mteja binafsi, Kampuni, NGO nk) na aina ya huduma ambayo mteja atakuwa anatumia.  Utaratibu mzima na viambatanisho vinavyotakiwa vimeelezewa na mdhibiti na MIC na vitambulisho vinavyokubaliwa na mdhibiti tu ndivyo vitakavyokubaliwa. 

Ni Wateja hai pekee ndio wanaoweza kujisajili, na kutumia huduma ya Tigo Pesa. 

  • Unaweza kujisajili na Huduma za Tigo Pesa iwapo wewe ni mteja hai wa Tigo.
  • Mteja yeyote wa Tigo anaweza kujisajili na Huduma ya Tigo Pesa kwa kupitia Wakala yeyote wa Tigo Tanzania. 
  • Kitambulisho cha Taifa pamoja na namba yako ya Tigo vitahitajika ili kukamilisha Usajili.
  • Usajili unaweza kufanyika kupitia wakala yeyote wa Tigo Pesa aliyesajiliwa au Maduka ya Tigo. 

Kufanya Miamala

  • Mteja lazima aidhinishe muamala wa Tigo Pesa kwa kutumia Namba ya Siri, ambayo anaitengeneza wakati anafanya usajili au kwa njia zingine, ambazo tunaweza kuzibainisha mara kwa mara.
  • Baada ya kuanzisha akaunti ya Mteja, ataweza kufanya miamala ifuatayo:
    • Kuweka fedha taslimu kupitia wakala wa Tigo Pesa aliyeidhinishwa kupata fedha za kielektroniki (e-value) katika simu yake ambayo anaweza kutumia kufanya yafuatayo:
    • Kutuma fedha kwa Wateja wengine wa Tigo aliosajiliwa/ambao hawajasajiliwa au watumiaji Waliosajiliwa katika mitandao mingine
    • Kutoa fedha kwa wakala wa Tigo Pesa aliyesajiliwa.
    • Kununua muda wa maongezi wa Tigo (au kadri ambavyo itakuwa imebadilishwa hapo baadae na MIC Tanzania Public Limited Company)
  • Mteja pia anaweza kutumia fedha katika akaunti yake kulipia bili na kununua bidhaa na/huduma.
  • Miamala mingine ya usimamizi wa akaunti inaweza kufanyika pia kama vile kuangalia salio, kuangalia taarifa fupi ya akaunti, au kupata taarifa ya akaunti ya mwezi na kubadilisha namba yako ya Siri.
  • Mteja pia anaweza kufurahia huduma zote za kibiashara na mapendekezo yanayotolewa na Tigo au na washirika wake wengine.
  • Ada za miamala zinazohusiana na huduma yoyote ya Tigo Pesa huwekwa wazi kabla ya kutolewa kwa huduma yoyote. Kwa msaada wowote unaohitajika kuhusiana na ada, Mteja anapaswa kupiga simu bure kwenda huduma kwa wateja, kupitia 100, tembelea maduka ya Tigo, tembelea tovuti yetu ya www.tigo.co.tz, au tembelea wakala ambako ada zimebainishwa.
  • Kwa kutumia huduma za Tigo Pesa Mteja anakubali kwamba ameelewa ada au gharama zinazotozwa kwenye muamala
  • Mteja anapaswa kuhakikisha utimilifu na usahihi wa muamala wa kupokea fedha na kuhakikisha salio katika akaunti linaendana na muamala uliofanyika kabla ya kuondoka katika eneo la wakala.
  • Mteja anashauriwa kuhesabu fedha taslimu, pale ambapo anatoa fedha (kutoa fedha) na kuhakikisha kuwa salio lililobakia katika simu yake liko sahihi kulingana na muamala uliofanyika kabla ya kuondoka eneo la wakala.
  • Mteja hataweza kufanya muamala wowote itakapotokea kwamba Mteja hana salio la kutosha katika simu yake kufikia thamani ya muamala anaotaka kufanya jumlisha na gharama zinazotakiwa.
  • Ni jukumu la Mteja kuhakikisha kuwa taarifa za anayepokea fedha na kiasi kinachohamishwa kiko sahihi kabla ya kukamilisha muamala.  Tigo haitawajibika iwapo fedha zitakuwa zimetumiwa na mpokeaji asiye sahihi kwenye muamala uliofanyika kikamilifu. 
  • Miamala ina ukomo uliowekwa na kutangazwa na Tigo mara kwa mara kama ambavyo itakuwa imeelekezwa na mdhibiti. Muamala wowote unaozidi kiwango kilichowekwa hautashughulikiwa.
  • Kiasi cha fedha kitakachobaki katika akaunti kwa wakati fulani kitakuwa na ukomo uliowekwa na Tigo kama ambavyo imeelekezwa na mdhibiti.
  • Mteja anaweza kupata taarifa ya akaunti kwa kutumia Menyu ya USSD ya Tigo kwa ada inayohusika.
  • Huduma ya TigoPesa haipaswi kutumiwa kwa shughuli zozote za udanganyifu, uzembe au kwa shughuli zisizo halali. Mteja anakubali kwamba fedha ambazo zinahamishwa kupitia Tigo Pesa hazijapatikana kutoka katika njia zisizo halali kama ilivyofafanuliwa na Sheria kila mara kama vile Utakatishaji wa Fedha, Kufadhili Ugaidi, rushwa, hongo, au makosa mengine yoyote yaliyofafanuliwa nasheria za AML/CFT.
  • MIC haitakubali muamala iwapo:
    • Mteja hajasajiliwa au kuidhinishwa au kupewa ruhusa ya kutumia Huduma ya Tigo Pesa au pale ambapo idhini ya namna hiyo imeondolewa au imezuiliwa.
    • Kiasi cha Muamala kilichoombwa na Mteja kiko chini ya kiwango au juu zaidi ya kiwango cha miamala ya Tigo Pesa kwa mujibu wa taratibu zinazohusiska.
    • Mteja ameshapitiliza kiwango cha mwisho cha miamala ya Tigo Pesa kwa siku kwa mujibu wa taratibu.
    • Tigo inapofahamu kuwa Mteja anajihusisha na shughuli za kihalifu. 

 

  1. Gharama/Ushuru/Ada na Salio ambalo halijatolewa.
    • Wateja wanatozwa ada kwa kutumia huduma za Tigo Pesa kwa bei ambazo zimeainishwa/zinazotangazwa mara kwa mara na zinazobadilishwa kila wakati katika tovuti ya Tigo Tanzania na katika maeneo ya Mawakala.
    • Gharama zote na ushuru katika huduma zinategemeana na kodi inayohusika kwa mujibu wa kanuni na sheria.
    • MIC ina haki ya kubadilisha gharama na ushuru kama itakavyoona inafaa kwa kutoa taarifa ya awali kwa wateja.
    • Pale itakapokuwa inahusuka, gharama zitategemeana na kubadilika kwa thamani ya sarafu ya kigeni.
    • Mteja anaweza kuomba taarifa anazotaka kuhusu gharama za huduma wakati wowote kupitia kitengo cha huduma kwa wateja, piga 100 au kwenye maduka yetu yoyote ya Tigo.
    • Tigo haiwajibiki kwa gharama za huduma ambazo zinatolewa na washirika wake au makosa yoyote ya kisheria kwa mujibu wa sheria ya Tanzania 

 

  1. Usalama na Matumizi yasisyo Idhinishwa
    • Mteja anawajibu wa kutunza vizuri na kutumia vizuri namba yake ya siri na miamala yote inayofanyika katika Tigo Pesa kwa kutumia namba yake ya siri na atapaswa kutufidia kufuatia madai yoyote yaliyotolewa kuhusiana na miamala hiyo.  Kumbuka Tigo haiwezi kumuomba Mteja atoe namba yake ya siri kwa hali yoyote na katika hatua yoyote.
    • Mteja hapaswi kutoa namba yake ya siri ya Tigo Pesa kwa mtu yeyote kwa sababu yoyote ikiwemo wakala wa huduma kwa wateja, Wafanyakazi wa Tigo au Wakala wa Tigo Pesa. Pindi Mteja anapobainisha kuwa namba yake ya siri ya Tigo Pesa imejulikana, anashauriwa kubadili namba ya siri haraka kwa kutumia utaratibu uliobainishwa.
    • Inapotokea simu yako, Kadi ya Simu au Namba ya Siri imeibiwa au unataka kutoa taarifa za tuhuma za udanganyifu au shughuli zisizo halali, piga simu 100 (namba ya huduma kwa wateja) na fuata maelekezo. Tigo itasimamisha akaunti yako mara moja kadri itakavyowezekana.  Mteja ataendelea kuwajibika kwa miamala yote itakayofanyika mpaka pale ambapo akaunti itakapokuwa imesimamishwa.
    • Mteja atawajibika kwa miamala yote iliyofanyika kikamilifu na iliyoidhinishwa katika akaunti ya Tigo Pesa na hasara itakayopatikana.
    •  
    • Pale ambapo Mteja ataingiza namba ya siri isiyo sahihi Mteja atapatiwa nafasi tatu za kujaribu tena kuingiza namba ya siri iliyo sahihi, akishindwa akaunti ya Mteja itasitiswa. Ili kuweza kufungua tena akaunti yake, Mteja atapaswa kuwasiliana na kitengo cha Huduma kwa Wateja cha Tigo, kupitia namba 100 kwa msaada au kutembelea maduka ya Tigo.

 

  1. Kufunga Akaunti yako.
    • MIC itafunga akaunti ya Mteja iwapo itapokea ombi kutoka kwa Mteja.
    • MIC vile vile inaweza kufunga akaunti ya Mteja kuzuia shughuli katika akaunti au kusitisha uwezo wa kuingia katika akaunti kwa namna yeyote iwapo tutafahamu au hutilia shaka kuwa akaunti yako inatumika kwa shughuli za udanganyifu, uzembe au shughuli zisizo halali au iwapo tunapaswa kufanya hivyo kutii sheria.
    • MIC pia inaweza kufunga akaunti yako iwapo tutaamini kuwa umevunja vigezo na mashariti haya, unajaribu kuathiri mifumo yetu au unaingilia bila sababu huduma zozote zinazotolewa na sisi.
    • MIC itafunga akaunti yako iwapo hautatumia Kadi ya Simu kwa siku 90 mfululizo na fedha zote za kielektroniki zitahamishiwa katika akaunti ya tushikilia fedha. Mteja ataweza kupata fedha zake za kielektroniki kwa kutembelea yeye mwenyewe katika Kitengo Cha Huduma kwa Wateja cha MIC Tanzania na akiwa na ombi la kimaandishi na uthibitisho wa utambulisho wake.
    • MIC inaweza kufunga akaunti yako pale unapokuwa sio Mteja wa Tigo tena.
    • Baada ya kusitiswa au kutokuunganishwa kwa huduma za Fedha kwa Simu za Mkononi za Tigo, Mteja atalipwa jumla ya kiasi chochote katika akaunti yake kwa kutoa ada zinazostahili za uendeshaji wa akaunti za Tigo au Wakala wa Tigo baada ya kuthibitisha utambulisho.
    • MIC haitawajibika kwako kwa uharibifu wa moja kwa moja au usio wa moja kwa moja unaotokana na kutenda au kutokutenda kwa MIC au washirika wake ambao tunawajibika kwao, iwe inajitokeza katika mikataba, uvunjifu wa sheria au amri, iwapo tutasitisha akaunti yako kwa mujibu wa kifungu hiki. 

 

  1. KUSITISHWA KWA HUDUMA 
  • MIC inaweza kusitisha huduma yote au sehemu yake wakati wowote na pasipo kuwajibika katika hali zifuatazo.
    • iwapo MIC haiwezi kutoa huduma, kwa ujumla au sehemu yake, iwe kwa sababu zisizoweza kuzuilika au pasipo kukusudia.
    • iwapo leseni au mkataba ambao MIC inapata haki zake na uwezo wa kutoa huduma husika itakapokuwa imesimamishwa, kusitishwa au kuzuiliwa; au
    • iwapo usitishaji huo ni lazima ufanyike kuwezesha marekebisho yoyote, maboresho, matengenezo, uboreshaji au kazi za marekebisho kwa mujibu wa mfumo; au
    • iwapo mteja atakuwa ameshindwa kukidhi vigezo hivi na masharti; au
    • iwapo Mteja anatumia vifaa ambavyo vinakiuka au vinadhaniwa kukiuka haki za uvumbuzi za MIC au washririka wake wowote.
    • iwapo MIC itatoa taarifa kwa Mteja baada ya tukio hilo ambalo halikutegemewa litatokea kama ambavyo imeelezewa katika kifungu 7.1.1 na pia itatoa taarifa kabla ya tukio lolote lililotajwa katika kifungu 7.1.3
  • Iwapo huduma itasitishwa kwa sababu za makosa ya Mteja, Mteja atawajibika kwa MIC kwa uharibifu au hasara yoyote ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja iliyopatikana. 

 

  1. MAJUKUMU YA MTEJA

Mteja anakubali na kuahidi:

  • Kutotoa au kuhamisha huduma, Kadi ya Simu au namba binafsi ya simu kwa mtu mwingine yeyote pasipo idhini yakimaandishi ya MIC. 
  • Kwamba Mteja anathibitisha kwamba Kadi ya Simu na haki zake zitabakia kuwa mali isiyoweza kutolewa na isiyohamishika ya MIC wakati wote. 
  • Kwamba wakati wote Mteja atakuwa na wajibu na kuwajibika kwa MIC kwa matumizi sahihi na utunzaji wa Kadi ya Simu na namba ya siri. Katika hali ambayo Mteja atakuwa anaendelea kupuuzia matumizi ya Kadi ya Simu au namba iliyotolewa kwa muda wa siku 90, MIC inaweza kusitisha namba hiyo na kuitoa kwaajili ya kutumiwa na Mteja mwingine. 
  • Kwamba wakati wote Mteja atabakia kuwa na wajibu wa kutunza siri za taarifa zozote au taarifa zinazopokelewa au kusafirishwa na Mteja kwa kutumia Mtandao na Mteja anakubali kutoa taarifa kwa MIC haraka iwezekanavyo kuhusu matumizi yoyote yasiyoruhusiwa ya Kadi ya Simu au huduma. Mteja anathibitisha kwamba MIC haitawajibika kwa hasara ambayo Mteja atapata kutokana na matumizi ya huduma ambayo hayakuidhinishwa  au Kadi ya Simu bila Mteja kujua. 
  • Kwamba katika tukio la kupotelewa au kuibiwa kwa Kadi ya Simu iwe kadi ilikuwa katika simu au la wakati ilipopotea au kuibiwa Mteja ataifahamisha MIC kwa kutumia namba ya simu iliyotolewa au kwa kutembelea vituo vya mauzo vya MIC kuomba huduma zisitishwe au kuondolewa na hapo atapaswa kuthibitisha taarifa ya kupotelewa au kuibiwa kwa maandishi kwa MIC kwa kuambatanisha na ripoti ya polisi kuthibitisha upotevu au kuibiwa. 
  • Kwamba mteja atawajibika kikamilifu na atalipa MIC gharama za simu zote zitakazopigwa kwa kutumia Kadi hiyo ya Simu iwe simu kadi imeibiwa au imepotea na Mteja anapaswa kuilipa MIC fedha zote na bila lawama kwa ada yoyote ya wajibu, gharama za huduma au gharama ambazo zitakuwa zimeingiwa kwa sababu ya matumizi yoyote ya udanganyifu ya Kadi ya Simu au kwa sababu ya kuibiwa kwa Kadi ya Simu.
  • Katika tukio la kupotelewa au kuibiwa kwa Kadi ya Simu Mteja atabakia kuwa na wajibu na kuwajibika kwa MIC kama ilivyotanguliwa kusemwa kwa kutumia Kadi ya Simu mpaka tarehe ambapo akaunti ya Mteja ilisitishwa na MIC. 
  • Kufidia MIC kwa gharama zote ambazo MIC imezipata au inapata kwa sababu ya kufungua upya Kadi ya Simu kwa matokeo ya madai ya udanganyifu. 
  • Mteja anathibitisha na kuhakikisha kwamba ana uwezo wa kuingia katika makubaliano haya na kutekeleza majukumu yake kama ambavyo yameelezwa hapa. 
  • Mteja anaendelea kuhakikisha na kuthibitisha kwamba taarifa na maelezo yaliyotolewa kwa MIC ni ya kweli na ataifahamisha MIC mara moja kwa maandishi iwapo kutatokea mabadiliko yoyote na anakusudia kuipatia MIC taarifa au nyaraka zinazohitajika mara kwa mara. Isipokuwa pale ambapo taarifa za usajili wa Kadi ya Simu zimefanyiwa marekebisho kwa kufuata utaratibu uliowekwa, Mteja ambaye taarifa zake binafsi zimesajiliwa atabakia kuwa na wajibu wa shughuli zote zitakazofanyika kwa kutumia Kadi hiyo ya Simu na akaunti ya Tigo Pesa. 
  • Mteja atathibitisha kwamba uwajibikaji wao katika mkataba utakuwa wa pamoja na kadhaa, katika hali ambapo Mteja ni zaidi ya mtu mmoja. 
  • Mteja atathibitisha kwamba hatatumia huduma hii kwaajili ya shughuli za kihalifu au zisizofaa na atawajibika kwa athari zozote zitakazotokana na matumizi hayo ya kihalifu na yasiyofaaya huduma au Mtandao. 
  • Mteja anaifidia na kuichukulia MIC kuwa haina athari dhidi ya upotevu wowote, wajibu, vitendo, mashauri, madai, gharama, matakwa na uharibifu wote na wa aina yoyote, (ikiwemo wa moja kwa moja, usiyo wa moja kwa moja, maalumu au uharibifu utokanao na matokeo), na ikiwa ni katika hatua zinazohusiana na mkataba, uzembe au kitendo kingine chochote, kinachojitokeza kwa sababu ya au kwa kuhusuana na kushindwa au kuchelewa kwa utendaji wa huduma zilizotolewa, au matumizi ya Huduma.   
  • Kwa huduma ambazo zinahitaji namba ya siri kama vile Tigo Pesa, Mteja anakubali kutunza namba zote za siri katika hali ya usalama na kuhakikisha kuwa hakuna mtu mwingine atatumia Huduma kwa kutumia namba ya siri ya Mteja, na Mteja anaendelea kuthibitisha kwamba ana wajibu wakuhakikisha kwamba hakuna utumiaji usioidhinishwa unafanyika kwa kutumia namba ya Mteja ya siri na kwamba Mteja atawajibika kwa shughuli zote zitakazofanyika kufuatana na matumizi hayo na hasara yoyote itakayojitokeza iwe imeidhinishwa au hapana. 

 

  1. MAJUKUMU YA MIC 
  • MIC inakubali kwa mujibu wa Vigezo na Masharti haya kutoa Kuduma kwa MTEJA. 
  • MIC itatoa ramani ya mtandao wa huduma kuonyesha maeneo ambayo yameshafikiwa kwaajili ya MTEJA mara kwa mara. 
  • MIC itatangaza gharama na orodha za gharama zinazotumika kwenye huduma mara kwa mara. 
  • MIC itatunza kwa siri taarifa na mawasiliano ya Mteja isipokuwa kwa sababu zilizotolewa hapa au kama ambavyo itakavyokuwa imetolewa katika matakwa ya kisheria. 

 

  1. MAELEZO YA USIRI
    • MIC na makampuni yake yote yanayohusiana yana wajibu wa kutunza usiri wa taarifa binafsi za WATEJA Kuonyesha wajibu wa MIC, MIC imetengeneza Maelezo ya Usiri ili kuwasilisha malengo yake ya kutoa mchakato wenye ufanisi kwaajili ya  uhifadhi sahihi wa taarifa za siri na kukidhi matakwa ya sheria ambayo zinasimamia uhakiki, utunzaji na utoaji wa taarifa bianfsi. 
    • MIC imetekeleza teknolojia, sera na mchakato wenye lengo la kulinda usiri, uadilifu na upatikanaji wa taarifa binafsi za WATEJA. MIC itarekebisha na kuboresha hatua hizi kila wakati. MIC haitawajibika au kuhusika kwa namna yoyote kwa kuibiwa au kupotea kwa taarifa binafsi za mteja nje ya udhibiti wa MIC. 
    • MIC haisambazi taarifa zozote binafsi za MTEJA kwa mtu mwingine isipokuwa inapokuwa imeombwa na MTEJA au ikiwa inatakiwa kufanya hivyo kisheria. Kwaajili ya kuondoa mashaka na ufafanuzi, MIC inaweza kulazimika kutoa taarifa binafsi kwa lengo la kukidhi matakwa yoyote ya kisheria au matakwa ya mdhibiti ya sheria inayohusika. 
    • MIC ina haki ya kufanya marekebisho au kubadilisha Maelezo haya ya Usiri wakati wowote kutegemeana na sheria mpya ya Usiri. 
    • Ufuatiliaji au Uwekaji wa kumbukumbu ya mawasiliano ya WATEJA kama vile simu zilizopigwa au SMS utafanyika kama ambavyo imeelekezwa kisheria au kwa lengo la kibiashara kwa kiasi kinachoruhusiwa kisheria. 

 

  1. SHERIA ZINAZOSIMAMIA

Vigezo na Masharti haya yanasimamiwa na sheria ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika vipengele vyote. 

 

  1. MAMBO MBALIMBALI
    • Vigezo na Masharti haya yanaweza kugawika, kwamba iwapo kifungu chochote kitabainishwa kuwa sio cha kisheria au hakiwezi kutekelezwa kisheria na mahakama yoyote yenye uwezo, basi kifungu hicho kitachukuliwa kuwa kimefutwa bila kuathiri vifungu vya kanuni vinavyobakia. 
    • Kushindwa kwa MIC kutekeleza haki yoyote mahususi au utoaji wa vigezo na masharti haya haitachukuliwa kama kuondolewa kwa haki au kifungu hicho, isipokuwa iwe imethibitishwa na kukubaliwa kwa maandishi na MIC. 
    • Vigezo na Masharti haya, kama ambavyo yanaboreshwa na MIC kila mara yanabeba makubaliano kamili kati ya MTEJA na MIC pale ambapo makubaliano maalumu yatakuwa yamesainiwa kati ya MTEJA na MIC ambayo yana vigezo na masharti yanayofanana na haya vifungu vya vigezo na masharti hayo mahususi vitatumika katika tukio la mgogoro au kutofautiana. 

 

  1. Ufanye nini unapohitaji msaada
    • Kwa msaada zaidi kutoa Tigo, piga namba 100 ( Huduma kwa Wateja). Kwa maelezo zaidi kuhusu kurudisha muamala tembelea http://www.tigo.co.tz/sw/tigo-pesa/jihudumie
    • Katika hali ambayo kitengo cha Huduma kwa Wateja hawakuweza kukusaidia na unataka kupeleka mbele suala lako kwa barua pepe complain@tigo.co.tz, eleza wazi suala lako na wapi lilikotokea. 
    • Katika hali ambayo haukuridhika na huduma za Tigo kwa Ujumla au suala lako bado halijatatuliwa baada ya Uongozi wa Tigo kuingilia kati, unashauriwa kuwasiliana na TCRA au BOT.



Tafuta duka la Tigo